02/01/2026
JAMII FM YATANGAZA WASIKILIZAJI NA WACHANGIAJI BORA WA VIPINDI WA MWAKA 2025
Jamii FM Radio imetangaza msikilizaji na mchangiaji bora wa vipindi vyake kwa mwaka 2025, tukio hilo limefanyika jumatano Disemba 31, 2025 katika kituo cha kurushia matangazo Jamii FM Redio Mtwara.
Mkurugenzi wa Jamii FM Redio Bw. Swallah Said Swallah amemtangaza Ndg. Mambo Katani (mtoto wa Fatu Mohamedi Kumbuko) wa kijiji cha Rondo Ntene Halmashauri ya Mtama mkoani Lindi kuwa msikilizaji na mchangiaji bora wa kiume, wakati Bi. Amina Mkanjima (binti ya Mkanjim, mama wa Yanga, Mama Bakari Kitemwe) kutoka Manispaa ya Mtwara Mikindani kuwa msikilizaji na mchangiaji bora wa k**e.
Mkurugenzi wa Jamii FM, Bw.Swallah, amesema kuwa utaratibu huu ulianza mwaka 2024 na utakuwa endelevu. Kadri miaka inavyoendelea huku kituo kikiwa kinaboresha njia za kupata washindi na zawadi zinazotolewa.
Aidha akitaja mipango ya kituo, Bw Swallah ameeleza kuwa kuanzishwa kwa Jamii FM chini ya MTUKWAO Community Media lengo ni kuibua na kuchakata taarifa za kijamii ambazo mara nyingi huwa hazisikiki.
Uchaguzi huo ulifanywa kwa kushirikisha wa wasikilizaji wenyewe, kupitia ujumbe mfupi wa maandishi (SMS), ambapo walichagua msikilizaji bora wa k**e na wa kiume.
Wakizungumza washiriki wa mshindano hayo baada ya kutangazwa mshindi na kuwapatia zawadi wamesema ushindani huu umechochea ushirikiano kati ya wasikilizaji na kuwafanya wahisi kuwa sehemu ya kituo.
Kwa upande wake mshiriki wa shindano hilo Bi. Esta Jacob wa kijiji cha Mwenge Majengo na Bi. Sofia Mkomi wa Madaba Tandahimba, wamesema kitendo cha Jamii FM ni cha kuigwa na vyombo vingine vya habari, kwani kushirikisha wasikilizaji ni njia bora ya kutoa maoni na kuelewa ni taarifa gani jamii inahitaji na matukio yanayowahusu.
Jumla ya washiriki kumi na tano (15) walichaguliwa na wasikikizaji Kwa awamu ya mwisho ya mashindano huku wawili kati yao wakiibuka na ushindi ambapo washindi wote wamepewa zawadi ya radio (Subwoofer) yenye thamani ya shilingi Laki Moja na elfu hamsini (Tshs 150,000/=).
Naye meneja wa Redio Bw. Amua Rush*ta amewashukuru wasikilizaji wa Jamii FM Redio Mtwara kwa kuisiliza redio kwa mwaka 2025 na kuukaribisha 2026 Kwa kauli mbiu ya Mtaa Kwa Mtaa.