Matukio Halisi

Matukio Halisi Maendeleo ya Moshi

Utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM 2020-2025 Jimbo la Vunjo linaloongozwa na Mbunge Mhe. Dr. Charles Stephen Kimei ...
28/03/2023

Utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM 2020-2025 Jimbo la Vunjo linaloongozwa na Mbunge Mhe. Dr. Charles Stephen Kimei na Rais wetu Mpendwa Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan.

"Usambazaji wa Umeme wa REA III Makuyuni."

MIAKA 700 YA WACHAGGA - 59MAISHA YA KILIMANJARO BAADA YA UHURU WA TANGANYIKA 1961.Tumeweza kuona kwamba baada ya uhuru w...
19/12/2021

MIAKA 700 YA WACHAGGA - 59

MAISHA YA KILIMANJARO BAADA YA UHURU WA TANGANYIKA 1961.

Tumeweza kuona kwamba baada ya uhuru wa Tanganyika taratibu maendeleo ya Kilimanjaro yalianza kufifia na kudumaa kwa sababu ya udumavu wa taasisi za kiuchumi na kisiasa zilizokuwa zimejengwa, kuimarishwa na kuboreshwa zaidi kwa ajili ya kusukuma maendeleo ya Kilimanjaro kwa makusudi karibu miaka 40 kabla ya uhuru wa Tanganyika.

Taasisi hizi zilianza kudumaa, kutelekekezwa na baadaye zote kufutwa kabisa moja baada ya nyingine na serikali mpya ya awamu ya kwanza ya Tanganyika/Tanzania chini ya Rais Nyerere. Japo hili lilikuwa ni pigo kubwa kwa Kilimanjaro lakini wachagga waliendelea kupambana katika hali hiyo hiyo ya udumavu huku taasisi muhimu za uongozi zikibadilika na mfumo uliokuja ni wa kuletewa viongozi kutoka kwenye serikali kuu tofauti na viongozi ambao wachagga waliwachagua wenyewe k**a ilivyokuwa inafanyika kabla ya uhuru wa Tanganyika.

Kwenye serikali ya awamu ya kwanza chini ya Rais Nyerere mambo yaliendelea hivyo lakini miaka michache baadaye sera ya serikali ilibadilika na kuzidi kujenga ukiritimba zaidi baada ya nchi ya Tanzania kuamua kufuata sera za kiuchumi na hata kisiasa za mrengo wa kushoto na mwaka 1967 likafanyika Azimio la Arusha ambalo lilikuwa azimio lililoweka sera kamili za kuiingiza nchi kwenye siasa na uchumi wa mrengo wa kushoto.

Sera za kiuchumi za mrengo wa kushoto ambazo msingi wake ni serikali kumiliki njia zote za kiuchumi zilikuja na mpango maalum wa kutaifisha biashara zote na mali zote zilizokuwa zinamilikiwa na taasisi binafsi pamoja na watu binafsi na kuzifanya ni mali ya serikali ambapo ilikuwa kila mtu anakabidhi biashara zake na kuiachia serikali kuziendesha.

Vitu k**a mashule yaliyokuwa yanamilikiwa na taasisi mbalimbali hasa taasisi za dini, vyuo vilivyokuwa vinamilikiwa na taasisi mbalimbali, mahospitali na vituo vya afya vilivyokuwa vinamilikiwa na taasisi binafsi, majengo makubwa, viwanda, maduka ya watu binafsi madogo kwa makubwa, mabenki na mashamba makubwa ya wafanyabiashara walioitwa “walowezi” na mashamba makubwa ya wachagga wenyewe ambapo tayari kuna ambao walikuwa wanamiliki mashamba makubwa na matrekta ya kisasa, vyote vilitaifishwa na serikali ya awamu ya kwanza chini ya Rais Nyerere.

Wakulima wakubwa wachagga na wageni huku wageni wengine wakiwa ni raia wa Tanzania waliondoka kwenye mashamba haya kupisha sera ya serikali ya utaifishaji wa mali zote ndani ya nchi baada ya Azimio la Arusha.

Mashamba haya yalikuwa yanafanya vizuri sana kabla ya huu utaifishaji lakini baada ya utaifishaji mashamba haya kwa sehemu kubwa yalitelekezwa na kudorora kabisa na serikali ilifanya haraka sana katika utaifishaji huu licha ya kwamba baada ya utaifishaji haikueleweka kwa nini serikali iliharakisha sana kuyataifisha huku ikiwa haina mpango wowote mkubwa wa maana wa kuyaendeleza, zaidi ilionekana ni k**a inataka tu kuhakikisha inakamilisha adhma ya kuifanya nchi kuwa ya kijamaa.

Serikali ya awamu ya kwanza iliyokuwa inaongozwa na Rais Nyerere iliamini kwamba inahitaji kumiliki njia zote za uchumi kwa kutaifisha biashara zote ndani ya nchi ili iweze kutoa huduma kwa usawa kwa watu wote. Hii ilikuwa ni sera ambayo ilichukuliwa kutoka kwenye nchi zilizokuwa na sera ya mrengo wa kushoto iliyopata umaarufu k**a siasa za kijamaa na kikomunisti.

Hata hivyo kwa upande wa mashamba makubwa hata baada ya serikali ya awamu ya kwanza kuyataifisha kwa sehemu kubwa haikufanya chochote zaidi ya kuyatelekeza kwa miaka mingi kukiwa hakuna chochote kinachofanyika. Baadaye baada ya mashamba haya kueguka kuwa mapori bila kuwa na uzalishaji wowote wa maana yalikuja kugawanywa kwa vyama vya msingi vya ushirika vilivyoaminiwa kwamba viko kijamaa na vitafufua kilimo katika mashamba haya. Lakini hata hivyo kwa sababu ya changamoto mbalimbali vikiwemo kukosekana kwa mitaji, maarifa na uzoefu, vyama hivi navyo vilishindwa kufufua mashamba haya pia.

Baada ya utaifishaji wa mali zilizokuwa zinamilikiwa na sekta binafsi kupitia taasisi binafsi na watu binafsi serikali ya awamu ya kwanza iliongeza wigo wa kutoa huduma za elimu na afya bila malipo kwa wananchi walio wengi. Hata hivyo kutokana na serikali kukosa uzoefu wa uendeleshaji wa biashara ambazo ilizichukua kwa watu na taasisi binafsi na kutokana na mambo kuendeshwa kisiasa na kiserikali kwa namna ya kutafuta umaarufu wa kisiasa mambo yalianza kwenda kombo huku wakurugenzi na maafisa wa serikali wakitumbukia kwenye vitendo vya rushwa iliyokithiri.

Watu wengi hasa wa vijijini walianza kupata changamoto kupata huduma hizi zilizoanza kutolewa na serikali k**a ununuzi wa vitu kwenye maduka na huduma nyingine kwenye taasisi nyingine k**a kwenye mashule na mahospitali kwani ilihitaji kujuana au kutoa rushwa kwa maafisa hawa ili kuweza kupewa kipaumbele kutokana na uhaba ulioanza kujitokeza uliotokana na ukiritimba wa serikali yenyewe.

Uhaba huu uliotokana na ukiritimba ulioambatana na rushwa iliyokithiri ilipelekea kukosekana kwa pembejeo muhimu na huduma nyingine kwa wakulima wa kahawa Kilimanjaro na kuzidi kudidimiza na kudumaza ustawi wa Kilimanjaro ambao bado ulikuwa unategemea sana zao la kahawa.

Rushwa iliendelea kutawala kwa kiasi kikubwa na kudhoofisha mambo mengi sana Kilimanjaro kuanzia elimu, afya, kilimo, uchumi na mambo mengine yaliyokuwa yamepiga hatua kubwa kabla ya uhuru wa Tanganyika ambapo rushwa ilitawala kwenye kila taasisi ya serikali ambayo ndio ilikuwa inatawala Kilimanjaro baada ya mifumo ya utawala iliyokuwepo kabla ya uhuru wa Tanganyika kufutwa.

Kipindi hiki ndio kipindi ambacho vigogo wa serikali walianza kuonekana ni watu muhimu na wa hadhi ya juu, kuogopwa na kuwa na sauti kubwa dhidi ya watu wengine ambao hawakuwa serikalini hasa katika nafasi za juu na haikuwa rahisi kushindana naye bila kujikuta kwenye matatizo.

Rushwa na ufisadi vilikithiri lakini kutokana na kwamba serikali haikuwa tayari kukiri kwamba kuna rushwa na badala yake kutumia propaganda kutangaza kwamba hakuna rushwa na serikali ya awamu ile ni safi na hakuna mtu aliyeruhusiwa kuongea kitu chochote kinyume na vile inavyotaka serikali huku vyombo vya vyote vya habari vikimilikiwa na serikali pekee, rushwa iliongezeka sana na kudumaza kabisa shughuli za kiuchumi na huduma za kiserikali pia.

Baada ya sera ya utaifishaji wa mali za taasisi binafsi sambamba na zile za watu binafsi kushindwa vibaya na kupelekea uchumi wa nchi kudorora sana, baadaye mwishoni mwa utawala wa awamu ya kwanza serikali ilirudisha baadhi ya biashara kwa watu binafsi zikiwa zimeporomoka kabisa na nyingi zikiwa hazina mitaji k**a zilivyokuwa nao wakati zinataifishwa na serikali ambapo nyingi zilikufa kabisa kwa kukosa mitaji.

Hata hivyo urudishwaji wa biashara hizi haukuzingatia zilipochukuliwa, zipo biashara nyingi ambazo zilipewa watu wengine kwa namna ya upendeleo na kujuana ili mradi kurudishwa kwa watu binafsi na zile zilizobahatika kurudishwa kwa wahusika zilirudi zikiwa zimefilisika kabisa na bila kuwa na mtaji wowote, na kwa sababu wakati zinachukuliwa wahusika hawakulipwa pesa yoyote ya fidia walirudishiwa hizi biashara wakiwa hawana mtaji na hivyo nyingi ziliishia kufa kwani hata biashara ya kahawa ambayo ndipo wachagga wengi walipatia huko mitaji ya kuanzisha biashara hizi ilikuwa imedorora sana na hivyo kukosa msingi wa mtaji wa kufufua tena biashara hizo. Kwa upande wa taasisi binafsi hasa taasisi za kidini nyingi zikiwa zimetaifishiwa mashule na mahospitali hazikurudishiwa mali zao isipokuwa shule chache sana.

Taasisi nyingi zinazotoa huduma za elimu na afya zilibaki kuwa ni za serikali mpaka leo kwa mfano chuo cha ualimu Marangu na vinginevyo. Mabadiliko pekee yaliyokuja kufanyika baadaye ni kutungwa kwa sheria ya kulinda mali za taasisi hizi ambapo taasisi za kidini na nyingine za binafsi ziliruhusiwa kujenga shule nyingine kwa mkataba kwamba serikali haitakuja kuzitaifisha tena k**a jinsi ilivyofanya mwanzo na kuziingiza taasisi hizi kwenye matatizo makubwa, uliopata umaarufu k**a Memorandum of Understanding(MoU).

Wachagga hawakuendana nayo wala kuipenda sera ya ujamaa kwa sababu kwanza kuanzishwa kwake kulidhoofisha zaidi vyama vya ushirika ambavyo vilikuwa na manufaa makubwa Kilimanjaro na baada ya muda vikafutwa kabisa. Pili sera hii ya ujamaa ilipelekea mali nyingi za wachagga kutaifishwa na serikali kwa namna ya k**a kunyang’anywa ambazo zilikuwa zimetafutwa kwa muda mrefu na kwa hali na mali na hivyo hata nje ya uchumi wa kahawa wachagga waliathirika zaidi kwenye biashara nyingine hivyo kupelekea uchumi wa Kilimanjaro kuanguka kabisa.

Hakuna mtu aliyejali mfumo uliokuwepo ulikuwa na faida kiasi gani wala ulikuwa na umuhimu kiasi gani, badala yake ilikuwa ni amri tu kwamba mali zote zitataifishwa na kufanywa za umma na kuendeshwa na serikali. Taasisi mbalimbali Kilimanjaro pamoja na wachagga wenyewe waliona wazi kwamba nchi inaenda kuangukia kwenye mfumo wa kikomunisti na kuona wazi kwamba Kilimanjaro inaenda kudhoofika sana.

Namna sera hizi za kijamaa zilivyokuwa zinatekelezwa wachagga walishindwa kuzielewa kabisa na kupata mtazamo hasi sana juu yake na kufikiri kwamba zimetengenezwa makusudi kuwaumiza na kuwasababishia msongo mkubwa wa mawazo.

Hata hivyo serikali ya awamu ya kwanza ilijaribu kutumia makanisa kujenga ushawishi kwa watu kuukubali ujamaa. Rais Nyerere mwenyewe alitumia kanisa na viongozi wa dini kueneza propaganda za sera za ujamaa kujaribu kupunguza mtazamo hasi juu ya ujamaa ili kuwaondoa watu wasiwasi kwamba hakukuwa na agenda za siri zilizojificha katika kuibadilisha nchi kuwa ya kikomunisti.

Hata hivyo bado hiyo haikutosha kuwashawishi wachagga kuukubali ujamaa baada ya kuwa biashara zao zote mpaka biashara ndogo ndogo kabisa mitaani na vijijini zikiwa zimetaifishwa na serikali huku wao hawajalipwa hata fidia na badala yake zimechukuliwa na maafisa wa serikali na badala yake sasa wanapata huduma kwa shida sana na hata wakati mwingine kulazimika kutoa rushwa kwa biashara ambazo zilikuwa ni za kwao wenyewe.

Vyama vya ushirika vikiwa vimefutwa na kuletwa taasisi nyingine kutoka serikali kuu ambao hawakuwa wana uelewa wowote mpana juu ya vyama hivyo na uzoefu wa kilimo hususan cha kahawa. Hiyo ilipelekea wakulima walipohitaji ushauri wa kitaalamu walijikuta wakulima wenyewe wana uwezo mkubwa na uelewa mpana wa kitaalamu kuliko hata wale walioletwa na serikali kuu kwa jukumu hilo, badala yake maofisa wengi wa serikali walijikuta wanageuka kuwa wabadhirifu na wala rushwa.

Tabia ya uvivu na kutojali ilishika kasi sana na wasimamizi waliokuwa wameletwa na serikali kuu ya Tanzania hawakuwa wanajali sana kazi hizo wala kuwa na shauku yoyote nazo na badala yake walijikuta wanashinda maofisini wakipiga hadithi na wengine kuamua kwenda kujishughulisha na biashara zao mbalimbali ili kuweza kupambana na hali ya maisha wakati huo mishahara yao ikiwa ni duni sana.

Hali hii ya uzembe na uvivu wa watumishi wa serikali ndio ilikuwepo miaka ya baada ya uhuru wa Tanganyika tofauti na kipindi cha Mangi Mkuu ambapo watu walikuwa wanajua lengo lao kiuchumi na wengi wakiwa sehemu ya kunufaika na kilimo biashara cha mazao hususan zao la kahawa basi walikuwa wakihamasika sana kuweka bidii kubwa na hivyo hakukuwa na uzembe wala uvivu wa kiasi hiki.

Wakati wa kipindi cha utawala wa Mangi Mkuu kazi zilifanyika kwa kujituma sana bila kisingizio wala kujali ugumu wa mazingira ya kazi lakini baada ya uhuru wa Tanganyika maofisa wapya walioletwa na serikali kuu walikuwa hawaishi visingizio hasa kusingizia kwamba hawana vifaa k**a vile usafiri au vitu vingine muhimu na hivyo maofisi yakageuka zaidi kuwa maeneo ya kwenda kupumzika badala ya kufanya kazi.

Ofisi hizi ambazo wakati wa utawala wa Mangi Mkuu zilijikita zaidi kwenye kufanya kazi zikiongozwa na kauli mbiu mbalimbali za kazi, lakini baada ya uhuru wa Tanganyika na viongozi kuletwa kutokea maeneo mengine siasa za itikadi zilianza kushika kasi na watu kuongea na kusambaza propaganda za chama na serikali ya awamu ya kwanza ikawa ndio tabia mpya inayojijenga na inayowapa watu kujulikana na kupandishwa vyeo au kupelekwa kwenye fursa kubwa zaidi hasa baada ya Azimio la Arusha.

Azimio la Arusha ndio lilikuja na ari kubwa zaidi katika kufanya propaganda na kutukuza itikadi ya chama na kutukuza viongozi na fikra za viongozi hasa Mwenyekiti wa chama Rais Nyerere ambapo kulikuwa na kauli mbiu kabisa ya kwamba "zidumu fikra za Mwenyekiti" badala ya kuweka “fokasi” kwenye kazi na kufuata ushauri wa wataalamu na sio maneno ya siasa.

Taasisi zote ambazo zilijengwa na wachagga kwa hali na mali kwa zaidi ya miaka 40 kabla ya uhuru wa Tanganyika na kuleta mabadiliko na maendeleo makubwa Kilimanjaro na ambazo ndizo zilizokuwa msingi wa maendeleo makubwa Kilimanjaro hazikuwahi kuonekana k**a zina maana yoyote wala kukubalika, zaidi ya kuishia kudhoofika na baadaye kufutwa kabisa. Sera zilizotekelezwa ni zile ambazo zililetwa na serikali kuu ya Tanzania.

Watu walioletwa Kilimanjaro kwa ajili ya utekelezaji wa sera hizo hawakuwa na uwezo wala uzoefu wa namna mambo yalikuwa yakifanyika Kilimanjaro na hivyo zile huduma mbalimbali kwa wakulima(extended services) zilizokuwa zinatolewa kipindi cha Mangi Mkuu vijijini ni k**a zilipotea kabisa na wakulima Kilimanjaro walipohoji au kuhitaji huduma hizo kwa ajili ya kuhakikisha mavuno yanakuwa yenye ubora wa viwango sahihi waliitwa wavivu, wazembe, wasio na uzalendo na wenye mitazamo ya kikoloni.

Hii iliwakatisha sana tamaa wachagga na hawakuwahi kuiamini serikali ya Tanganyika/Tanzania ambayo iliwakuta kwenye mafanikio makubwa na kasi kubwa ya kimaendeleo kuelekea kwenye utajiri na kudororesha uchumi na kuwarudisha nyuma kwenye hali ngumu ya maisha na hivyo kupelekea wachagga kujenga mtazamo kwamba sera yoyote ya serikali inayokuja Kilimanjaro ina lengo baya la kuwaumiza na kuwadhoofisha. Katika nyakati hizi hizi ilianzishwa sera ya serikali ambayo huwa ni maarufu k**a “quota” juu ya ufaulu wa wanafunzi wanaojiunga na elimu ya sekondari.

Sera hii ilikuja na hoja kwamba Kilimanjaro watu wameshasoma na hivyo hawapaswi kupewa kipaumbele na badala yake wanatakiwa wasubiri watu wa maeneo mengine ya Tanzania wasome kwanza. Hivyo alama za ufaulu kwa watu wa Kilimanjaro zilipandishwa kufikia angalau 85% ili kuweza kuchaguliwa kujiunga na elimu ya sekondari wakati huo mikoa mingine watu walihitajika kupata angalau 55% kuweza kuchaguliwa kujiunga na elimu ya sekondari.

Sera hii ilijumuisha shule za sekondari zilizokuwepo Kilimanjaro ambazo ndio zilikuwa nyingi zaidi kuanzia zile zilizojengwa na wachagga wenyewe kupitia KNCU mpaka zile ambazo zilikuwa zinamilikiwa na taasisi za kidini Kilimanjaro ambazo pia zilijengwa na wachagga kwa kushirikiana na viongozi wa dini lakini zikataifishwa na serikali ya awamu ya kwanza na serikali kugoma kabisa kuzirudisha kwenye taasisi binafsi zilikotaifishwa.

Serikali ya awamu ya kwanza iliyoongozwa na Rais Nyerere ilikuja na hoja hii kwamba mikoa mingine inatakiwa iendelee kwanza kuifikia Kilimanjaro tuwe sawa ndio fursa zirudi kawaida kwa hivyo Kilimanjaro italazimika kupunguza kasi ya maendeleo mpaka hayo maeneo mengine ya nchi yaendelee kwanza na watu wa huko wasome kwanza kufikia kiwango cha Kilimanjaro, japo hata hivyo haikujulikana ni lini muda huo utafika kwani hakuna tarehe kamili iliyopangwa kwamba mpaka mwaka fulani.

Kwa bahati mbaya zaidi hakukuwepo hata na mbadala wala shule binafsi ambazo watu wangeweza kusoma baada ya kukosa fursa kwenye sekondari za serikali kwani serikali ilikuwa imetaifisha shule zote ikiwa ni pamoja na zile za dini zilizokuwepo Kilimanjaro pamoja na zile zilizojengwa na wachagga wenyewe kupitia KNCU na hivyo wachagga walilazimika kufuata maamuzi ya serikali juu ya sera hii ambayo wenyewe waliiona k**a sera iliyotungwa ili kuwabagua na kuwarudisha nyuma kimaendeleo kwa makusudi. Wachagga walijiona kwamba ni k**a wanapewa adhabu kwa kosa ambalo hawajafanya wao, kwa sababu wao hawahusiki chochote kwa maeneo mengine ya nchi kuwa nyuma kimaendeleo.

Wachagga waliona kwamba huu ni k**a mpango ovu uliopangwa dhidi ya wachagga na Kilimanjaro na sera hii ya serikali ya awamu ya kwanza waliiona kuwa imejaa ubaguzi ndani yake na lengo lake lilikuwa ni kuwakomoa wachagga na kuwanyima elimu kwa kipindi kirefu kisichojulikana. Wakati wachagga wanaiona sera hii k**a sera ya kibaguzi na inayowaumiza, maeneo mengine ya nchi waliifurahia na kuiona iko sahihi kwa sababu haikuwa inawaumiza lakini kwa kuwa ndio wengi na wanaoipa nguvu serikali na zaidi kupitia propaganda za serikali ya awamu ya kwanza, sera hii ilipata uhalali wa kupitishwa na kuingizwa kwenye utekelezaji.

Wachagga walitegemea fursa ziwe sawa kwa kila mtu na sio kupitisha sheria zinazoleta ubaguzi na kuwanyima fursa watu wenye uwezo mkubwa wanaotokea Kilimanjaro huku watu wenye uwezo wa kawaida kutoka maeneo mengine ya nchi wakipewa nafasi.

Hata hivyo baada ya sera hii kuingizwa kwenye utekelezaji wachagga wengine waliamua kubuni mbinu mbadala kukabiliana na sera hii ya serikali ya awamu ya kwanza iliyokuwa inabagua wachagga kwenye eneo la elimu ambayo waliifanya kimya kimya. Mikoa mingine ilikuwa na utoro mkubwa wa wanafunzi na hivyo kwa kujua kwamba kupata alama za ufaulu ukitokea mkoa wa Kilimanjaro imekuwa ni changamoto, kwa siri wachagga walianza kualikwa kwenda kununua nafasi hizi zilizokuwa zinaachwa wazi kwenye mikoa mingine kwa sababu ya utoro wa wanafunzi.

Hivyo mikoa hii ambayo ilikuwa na utoro mkubwa kwa sababu mbalimbali k**a vile binti kuolewa akiwa bado yuko shuleni, vijana kutakiwa kwenda machungani na sababu nyinginezo zilizopelekea nafasi nyingine kupatikana wachagga wengi walizinunua na kuzitumia. Kwa sababu ufaulu kutoka mikoa hii kwenda sekondari ulikuwa rahisi wachagga wengi waliochukua hatua kununua nafasi hizi kwa kuingia maelewano na wakuu wa shule hizo na kusoma kwenye mikoa mingine wengi waliweka bidii kubwa sana kwenye masomo na walifaulu na kuendelea na masomo ya sekondari, tofauti na Kilimanjaro ambako ni wanafunzi wachache sana walikuwa wanafaulu na mara nyingi shule nyingi zilikuwa zinatoa kapa bila kufaulisha hata mwanafunzi mmoja kutokana na alama za ufaulu kuwekwa juu sana kwa wanafunzi wanaotokea Kilimanjaro.

Hata hivyo haikuchukua muda mrefu wachagga waliokuwa wananunua nafasi hizi ili kusoma kwenye mikoa mingine walianza kugundulika kwamba kuna ujanja wanatumia. Kwa sababu taarifa zilipelekwa kwenye uongozi wa juu kwamba wanashangaa kuona kwamba majina ya ukoo wa kichagga k**a Lyimo, Shayo, Mrema, Kileo, Massawe n.k. wanatokea mikoa mingine kwa wingi isivyo kawaida katika kuchaguliwa kwenda Sekondari. Ilikuwa inawashangaza kuona watu wa ukoo wa Shirima kutokea mkoa wa Mtwara au Lindi au mtu wa ukoo wa Mushi anatokea mkoa wa Tabora, ndipo walipoanza sasa kufuatilia watu kwa majina yao ya ukoo kuhakikisha kwamba wachagga hawapigi chenga na kupita njia mbadala ili kusoma sekondari k**a walivyokuwa wanafanya.

Baada ya mbinu hii ya wachagga kununua nafasi kwenye mikoa mingine ili kurahisisha kupata fursa ya kujiunga na elimu ya sekondari kujulikana, wachagga walikuja na mbinu nyingine mpya ya kununua jina la mtu wa mkoa husika na kulitumia k**a lilivyo ambapo hapa wachagga walilazimika kujitahidi sana kuficha utambulisho wao halisi kwa hali na mali ili wasijulikane kwamba wametokea mkoa wa Kilimanjaro na walihakikisha majina bandia waliyokuwa wananunua ndio majina pekee yanayojulikana.

Mbinu hii ya kutumia majina bandia ya watu wa mikoa mingine iliwasaidia sana wachagga kuendelea kielimu katika mazingira ambayo yaliwabana sana kwenye fursa za elimu. Lakini hata hivyo bado sio wote wamefanikiwa kupona moja kwa moja kwenye mbinu hii ya kutumia majina ya wengine kwani wengi ndio hao waliokuja kushutumiwa kuwa na vyeti feki na serikali ya Magufuli ya awamu ya tano na kufukuzwa kazi bila kulipwa mafao yao. Wengi zaidi walioumia katika sakata hilo la vyeti feki walikuwa ni wachagga na wengi walinunua majina hayo kipindi hicho cha awamu ya kwanza chini ya Rais Nyerere kutokana na sera ya elimu iliyowagua na kuwabana.

Hata hivyo baada ya sera za ujamaa zilizoletwa Tanzania na serikali ya awamu ya kwanza kufeli vibaya sana hasa kuanzia miaka ya 1970’s na 1980’s na kusababisha anguko kubwa sana la uchumi Tanzania na mambo mengi kudorora sana Rais Nyerere alikubali kuachia madaraka baada ya kukaa madarakani kwa karibu miaka 25 na kumpisha madarakani Rais Ali Hassan Mwinyi.

Rais Ali Hassan Mwinyi japo alirithi mifumo iliyojaa ukiritimba wa serikali ambayo haikuwa mizuri kwa ukuaji wa uchumi kutoka kwa Nyerere lakini Mwinyi yeye alikuja na sera nzuri za kuchochea ukuaji wa kiuchumi kwa kupunguza sana ukiritimba wa serikali katika kuhodhi njia za uchumi na kuruhusu sekta binafsi kuanza kukua tena kupitia taasisi binafsi kuanza kujijenga katika kumiliki njia za kiuchumi.

Sera nyingi zilizokuwa zinakwamisha maendeleo ya kiuchumi kwa mfumo wa uchumi kumilikiwa na serikali na kusababisha mdororo mkubwa wa kiuchumi wakati wa awamu ya kwanza ya Rais Nyerere ziliondolewa kwa kiasi kikubwa na hivyo taratibu uchumi wa nchi ulianza kukua tena na biashara Kilimanjaro zilizokuwa zimepoteza kabisa mwelekeo zilianza kupata matumaini japo wachagga wengi walikuwa wamepoteza ile ari ya maisha, matumaini makubwa ya kimaendeleo na mapambano makubwa waliyokuwa nayo kabla ya uhuru na miaka michache ya mwanzoni baada ya uhuru wa Tanganyika.

Taasisi za kidini zilianza kujenga tena taasisi binafsi za elimu, vituo vya afya na huduma nyingine za kijamii kwa kasi Kilimanjaro. Baada ya kuruhusiwa kujenga tena taasisi hizi wachagga walianza tena uhamasishaji wa kujenga mashule ya sekondari hasa kupitia taasisi binafsi kwa kasi ili kukabiliana na changamoto ya ukosekanaji wa shule mbadala za sekondari.

Mwaka 1992 ilipitishwa sera ya demokrasia ya vyama vingi ambayo ilizidi kujenga matumaini zaidi ya kisiasa na kiuchumi kwa Kilimanjaro na hivyo watu walizidi kuwekeza katika kuhakikisha zilipatikana shule nyingi za kutosha uhitaji kadiri ya watu watakavyoweza kumudu gharama. Wachagga pia walikuwa mstari wa mbele sana katika kuanzisha vyama mbalimbali vya kisiasa Tanzania baada ya fursa hiyo kujitokeza tena mwaka 1992 baada ya zaidi ya miaka 30 ya utawala wa kiimla wa chama kimoja.

Licha ya serikali kugoma kabisa kurudisha shule na taasisi nyingine ilizotaifisha kutoka kwa taasisi za kidini pamoja na kwamba taasisi hizi ziliiomba na kuisihi sana serikali kurudishiwa taasisi zao ilizozitaifisha na kugomewa, lakini hata hivyo haikuchukua muda mrefu Kilimanjaro ilianza tena kupata umaarufu wa kuwa na shule nyingi zinazofanya vizuri sana na wazazi wengi kutoka maeneo mbalimbali ya nchi ya Tanzania walijenga mtazamo kwamba Kilimanjaro kuna elimu nzuri na wale wenye uwezo wengi walipeleka watoto wao kwenda kusoma Moshi.

Baada ya sera za serikali ya awamu ya pili Tanzania chini ya Rais Ali Hassan Mwinyi kuanza kuruhusu taasisi binafsi kuanza kutoa huduma mbalimbali k**a elimu, afya n.k.,. na taasisi hizi kuanza kujengwa tena kwa kasi Kilimanjaro wachagga walipata matumaini mapya ya kusonga mbele kupitia elimu ambayo ilikuwa imekuwa changamoto sana kwao kwenye serikali ya awamu ya kwanza Tanzania chini ya Rais Nyerere iliyokaa madarakani karibu miaka 25.

Hata hivyo kwa mujibu wa Dr. Reginald Mengi kwenye kitabu chake cha “I can, I must and I will” anasema kwamba mwaka 1989 baada ya yeye na wawekezaji wengine ndani ya nchi kuwa wameanza kupata mafanikio makubwa Nyerere alijaribu kumshawishi Rais Mwinyi arudishe tena sera za Ujamaa k**a yeye alivyofanya akiwa madarakani na hivyo watu walioanza kutajirika mali zao zitaifishwe tena na kufilisiwa.

Dr. Reginald Mengi anasema kwamba Nyerere alidai kwamba ubepari na unyonyaji unarudi tena na kutolea mfano kiwanda chake cha vinywaji baridi cha Bonite Bottlers Co. Ltd kilichopo mjini Moshi mkoani Kilimanjaro k**a mfano wa ubepari wa kimarekani ambao yeye binafsi anaamini ni mbaya na wa kinyonyaji. Mfanyabiashara Reginald Mengi anasema kwamba yeye pamoja na wawekezaji wenzake waliogopa sana.

Hata hivyo Nyerere alipendekeza haya bila kujali kwamba sera zake za ujamaa wa serikali kutaifaisha mali za taasisi binafsi na watu binafsi na kuhodhi njia zote za kiuchumi zilisababisha kutokea kwa njaa, umaskini mkubwa na uhaba mkubwa wa bidhaa uliopelekea watu kukosa hata mahitaji ya kawaida ya kila siku na uchumi wa nchi kuanguka vibaya sambamba na nchi kukumbwa na madeni makubwa ambayo yamekuwa mzigo kwa nchi mpaka leo.

Hata hivyo kwa mujibu wa Reginald Mengi Rais Mwinyi alikataa kabisa pendekezo hilo la Nyerere jambo lililopelekea kutokea kwa mvutano mkali na kurushiana na maneno makali kati ya Mwinyi na Nyerere kwenye mkutano wa chama na hiyo ikawa moja kati ya sababu ya Nyerere kuamua kujiuzulu uenyekiti wa chama. Endapo Rais Mwinyi angekubaliana na pendekezo hili la Nyerere ni wazi kwamba mambo yangekuwa magumu tena na hatua ambayo Kilimanjaro ilikuwa imeanza kupiga kwenye kujenga tena upya taasisi zinazotoa huduma muhimu za kijamii lisingekuwa limefanyika au kufanyika kwa kiwango kidogo k**a wangekuja kuruhusu tena baadaye.

Japo wachagga mpaka leo bado hawajaweza kupata uongozi wa wazawa uliokuwa na mafanikio makubwa lakini ukafutwa baada ya uhuru wa Tanganyika na serikali ya awamu ya kwanza lakini wameendelea kupitia taasisi binafsi na taasisi za kidini kujenga taasisi zaidi za kutoa huduma mbalimbali za kijamii mpaka sasa na vyuo vikuu mbalimbali vimeendelea na vinaendela kufungua matawi zaidi Kilimanjaro katika kutanua zaidi wigo wa elimu ya juu.

Kupitia taasisi binafsi wachagga wamejaribu na wanaendelea kupambana kuwekeza kwenye teknolojia ya habari na mawasiliano na hata ujasiriamali na hizi zimesaidia sio wachagga peke yake bali hata watanzania kwa ujumla wameendelea kunufaika na taasisi hizi.

Licha ya taasisi mbalimbali za kitaaluma kuendelea kuongezeka Kilimanjaro na wachagga mbalimbali kutoka Kilimanjaro kuendelea kubobea katika fani mbalimbali na kuendeleza uwezo mkubwa unaonufaisha taasisi mbalimbali maeneo mbalimbali duniani bado Kilimanjaro haijaweza kuja na mpango sahihi wa kuinua uchumi wa Kilimanjaro kwa viwango vya juu k**a ilivyotokea kipindi cha Mangi Mkuu.

Ukweli ni kwamba hili sio jambo linaloweza kutokea kiurahisi k**a jinsi lilivyotokea wakati wa serikali ya Mangi Mkuu kwa sababu za kimifumo pengine pamoja na za kisiasa lakini bado kuna namna nyingine nyingi za kusaidia kurudisha maendeleo na utukufu wa Kilimanjaro uliopotea bila kutegemea kupitia mifumo ya kiserikali moja kwa moja ambayo hata ukisema uitegemee itaishia kukuangusha na kujikuta mnaishia kwenye mitego ya kisiasa na kukwama.

Chama cha ushirika cha KNCU ambacho kilifanya makubwa sana zamani hasa miaka ya kabla ya uhuru wa Tanganyika kilikuja kufufuliwa na kiko hai hata sasa lakini hakiwezi kufanya tena makubwa k**a kiliyofanya zamani kwa sababu mbalimbali zikiwezo za kisiasa na kiutendaji lakini kubwa zaidi ni kukosa nia na maono na kushindwa kujenga imani na matumaini kwa wanachama ambayo yanahitaji kuongezewa nguvu na mipango na mikakati sahihi inayoongozwa na nia njema.

Ahsanteni.

CREDIT@ URITHI WETU WACHAGGA FACEBOOK PAGE. 👏👏👏🔥🔥

MIAKA 700 YA WACHAGGA - 58ANGUKO LA MIFUMO YA UTAWALA KILIMANJARO.ELIUFOO SOLOMON, KIBARAKA WA CHAMA CHA TANU ALIYETUMWA...
18/12/2021

MIAKA 700 YA WACHAGGA - 58

ANGUKO LA MIFUMO YA UTAWALA KILIMANJARO.

ELIUFOO SOLOMON, KIBARAKA WA CHAMA CHA TANU ALIYETUMWA KUIDHOOFISHA KILIMANJARO.

Miaka ya 1950’s wachagga tayari walikuwa wamejenga mifumo imara sana ya kiuchumi na kisiasa kwa zaidi ya miaka 30, tangu miaka ya 1920’s na tayari walikuwa mbele sana kimaendeleo ukilinganisha na jamii nyingine Afrika kwa nyakati hizo.

Kufikia miaka ya 1950’s wachagga walikuwa kati ya jamii zinazojitambulisha k**a nchi au taifa japo hawakuwa wamepata uhuru kutoka kwa Waingereza lakini wakiwa wamepiga hatua kubwa kiuchumi na kuimarisha taasisi za kiuchumi na kiutawala wakiendelea kupiga hatua kwa kasi kubwa.

Ni katika miaka hii ya 1950’s wakati wachagga tayari hata kisiasa wakiwa wameshakomaa sana ndipo maeneo mengine hususan makao makuu ya serikali ya kikoloni Dar es Salaam ambapo watu walikuwa wanaendelea kuimarisha harakati za kudai uhuru wa Tanganyika yote.

Harakati hizi za uhuru wa Tanganyika kupitia vyama mbalimbali k**a chama cha United Tanganyika Party(UTP), TAA na baadaye TANU ambacho kilianzishwa Dar es Salaam na kuenea baadhi ya maeneo ya nchi kilishindwa kuingia kujiimarisha Kilimanjaro kwa sababu wachagga walijiona tayari wao ni taifa na wana nchi inayofanya kazi kwa usahihi kabisa ikisubiri kupatiwa uhuru wake na hivyo hawakuhitaji taasisi nyingine yoyote inayofanya harakati za kupigania uhuru wa Tanganyika kuingia Kilimanjaro kwa sababu maisha yenyewe ya wachagga yalikuwa tayari ni mazuri na maendeleo yalikuwa yakienda kwa kasi kuliko eneo jingine lolote.

Kwa kuwa pia mfumo wa kisiasa ulikuwa imara hakuna mtu aliyejihangaisha na harakati nyingine za kisiasa zaidi ya siasa za ndani ya Kilimanjaro lakini zaidi wachagga walijihusisha na shughuli za kiuchumi na maendeleo ya Kilimanjaro.

Chama cha TANU kilipojaribu kuingia Kilimanjaro bila mafanikio na kuona kwamba aidha kinaweza kushindwa kukabidhiwa uhuru wa Tanganyika au kukabidhiwa uhuru wa Tanganyika huku Kilimanjaro ikiachwa nje ya Tanganyika ndipo kilitengeneza agenda ya siri ya namna kuidhoofisha Kilimanjaro kwa kutumia makada wa chama cha TANU kutoka Kilimanjaro waliokuwa nje ya Kilimanjaro kimasomo.

Eliufoo Solomon alikuwa ameshawishiwa kujiunga na tawi la TANU akiwa anasoma chuoni Makerere Uganda wakati huo kabla hajaenda kusoma Marekani na hivyo baada ya kutoka Marekani ilikuwa rahisi kumshawishi kujipenyeza ndani ya siasa za Uchaggani, Kilimanjaro akiwa k**a kada wa TANU na akifanya kazi kwa maslahi ya chama cha TANU badala ya maslahi ya wachagga Kilimanjaro.

Hivyo mara baada ya Eliufoo Solomon kuingia kwenye nafasi ya urais wa Wachagga na kutakiwa kutoa mwongozo kwa baraza la halmashauri kuu ya wachagga ndipo nia yake na agenda zake za siri alizobeba na chama cha TANU zilianza kuonekana wazi. Kwa wale waliopigia kura chama cha kiliberali cha (CDP) kwa kuvutiwa na sera zao dhidi ya chama kikongwe zaidi cha wachagga wahafidhina (KCCU) walikuwa na matarajio makubwa zaidi na matumaini makubwa zaidi ya ustawi wa Kilimanjaro kuliko kipindi kilichoisha cha Mangi Mkuu wa wachagga, lakini hata hivyo mambo yalienda tofauti na matarajio yao ambapo kimsingi ilikuwa ni kinyume chake.

Ilikuja kuwa wazi kwamba Eliufoo Solomon alikuwa anatumiwa na watu kutoka nje ya Kilimanjaro kwa maslahi yao akiwa k**a kibaraka na kada wa chama cha watu hao. Licha ya kampeni kubwa alizofanya kupitia chama cha CDP, Eliufoo Solomon hakuwa na maono yoyote ya kisiasa wala kiuchumi kwa wachagga Kilimanjaro na hakuwa na jambo lolote alilokuwa amepanga kusaidia juu ya wachagga katika mipango yake.

Baada ya kufanikisha alichokuwa ametumwa na watu wa kutoka nje ya Kilimanjaro aliacha kujihusisha na siasa za Kilimanjaro mara moja na pia kuacha kushiriki mikutano ya baraza la halmashauri kuu ya wachagga na hata kutelekeza ofisi aliyokabidhiwa na wachagga ya urais wa wachagga bila kusema lolote, kitu ambacho kilionekana ni usaliti mkubwa sawa na kosa la uhaini kwa wachagga.

Badala yake Eliufoo Solomon aliondoka na kuelekea Dar es Salaam kujihusisha na shughuli za chama cha TANU akiwa k**a kada wake na hivyo kuacha ombwe la uongozi akiwa k**a kiongozi mkuu aliyechaguliwa na wachagga Kilimanjaro.

Mfumo wa uongozi wa wachagga chini ya Mangi Mkuu wa wachagga na baraza la Halmashauri kuu ya wachagga ulikuwa ni mfumo bora sana wa kisiasa uliloleta mapinduzi makubwa ya kiuchumi na kisiasa na wa kupigiwa mfano ukilinganisha na sehemu yoyote Tanganyika na hata katika bara la Afrika, lakini waliokuwa wanafikiri kunahitajika mabadiliko ni watu ambao hawakuwa na uelewa mpana wa hatua kubwa ambayo wachagga walikuwa wamepiga kupitia mfumo huu.

Hivyo kitendo cha Eliufoo Solomon kutelekeza wachagga na kuwaacha kwenye mataa akiwa k**a Rais wa serikali ya wachagga ilikuwa ni kitendo cha kuhujumu mfumo uliokuwa na nguvu na uliokuwa na manufaa makubwa kwa watu wa Kilimanjaro.

Wachagga wengi na hasa watu wazima walikasirishwa sana na namna Eliufoo Solomon alivyofanya baada ya kupewa nafasi ya kuwa Rais wa wachagga na baadhi ya waliomuunga mkono kwenye harakati za mabadiliko walilalamika kwamba wametumika katika kumsaidia kufanikisha agenda zake binafsi.

Baadhi ya wazee waliomlaani na kumuona k**a msaliti na mhuni walisema sio kwamba walikuwa wanapingana na yeye kushiriki kwenye harakati za TANU bali namna alivyotumika na watu wa TANU alifanya wachagga waonekane ni wajinga, kwani angeweza kuchagua kimojawapo cha kufanya badala kuwafanya watu wajinga na kuwaacha kwenye mataa kwa sababu baada ya Mangi Mkuu aliyekuwa anajituma sana na aliyekuwa anapambana sana kwa ajili ya maendeleo ya Kilimanjaro kuondoka kwenye kiti hicho wachagga waliachwa njia panda kwani hakukuwa na kiongozi mwenye maamuzi ya mwisho wa kuonyesha njia.

Kitendo cha kwamba watu wa chama cha TANU walikuwa wakifanya kazi nyuma ya Eliufoo Solomon na chama cha CDP kikiwa k**a tawi dogo la TANU wakiwa na agenda za kuhujumu maendeleo ya Kilimanjaro moja kwa moja kwa maslahi yao binafsi hakikumpa nafasi Eliufoo ya kuweka akili yake katika maendeleo ya Kilimanjaro na kuishia kufanya kinyume chake.

Wazo pia la kuwa na Rais wa wachagga lilikuwa wazo geni kutoka nje ya Kilimanjaro, lisiloendana na tamaduni, mila na desturi za wachagga na ambalo wachagga wengi walikuwa bado hawawezi kulihisi k**a lina mamlaka fulani k**a jinsi lilivyokuja tofauti na cheo cha umangi ambacho ni cha asili ya wachagga kwa karne nyingi nyuma.

Hata madhara ya kukosekana kwa uongozi imara na thabiti Kilimanjaro yalianza kuonekana huku baraza la Halmashauri kuu ya wachagga likijiongoza lenyewe. Kukosekana kwa uongozi thabiti kulipelekea ari na hamasa kupungua kiasi na kasi ya maendeleo pia kuanza kupungua. Kilimanjaro ilikuwa ni sehemu ya mwisho ambayo chama cha TANU kilikubaliwa kuingia baada ya njama za kisiasa zilizosukwa kuangusha utawala wa Mangi Mkuu kufanikiwa na hivyo kuwa sehemu ya Tanganyika.

Wafuasi walipiga kura ya maoni kuunga mkono sera za chama cha CDP pamoja na wachagga kwa ujumla wakiwa na hamasa na matumaini makubwa kuliko siku bora zilizopita na kutegemea umoja zaidi, mshik**ano zaidi demokrasia na ustawi zaidi Kilimanjaro.

Lakini Eliufoo Solomon hakujihangaisha kuchukua muda kupitia sera zake na kuishauri serikali ya Tanganyika baada ya uhuru ambayo alipewa zawadi ya uwaziri wa elimu kutekeleza baadhi ya ahadi zake Kilimanjaro. Eliufoo Solomon alipaswa kufanya hivyo akishirikiana na baraza la Halmashauri kuu ya wachagga baada ya uhuru wa Tanganyika lakini badala yake alijikausha na kuendelea kufanya mambo mengine kabisa.

Hata mfumo wa utawala wa umangi ambao Eliufoo Solomon alitumika kuudhoofisha akishirikiana na chama cha TANU ambapo ulikuwa umeiletea Kilimanjaro maendeleo makubwa na ambao ulikuwa umeboreshwa na kuwa wa kidemokrasia kwa kiasi kikubwa sana mpaka kufikia miaka ya 1950’s ulikuja kufutwa mwaka 1962 mara baada ya waingereza kukabidhi uhuru wa Tanganyika kwa chama cha TANU na kuondoka.

Kulitengenezwa propaganda nyingi sana za chuki dhidi ya mfumo wa utawala wa umangi kwa ajili ya kuudhoofisha bila kujali kwamba mpaka kufikia miaka ya 1950’s mfumo wa utawala wa umangi ulikuwa tayari umeboreshwa sana na ulikuwa tayari ni mfumo wenye demokrasia kubwa na huru kuliko hata Tanzania ya leo.

Japo aliyekuwa Mangi Mkuu wa wachagga alipeleka kesi mahak**ani kuishtaki serikali juu ya kuondolewa kwa mfumo wa umangi na akashinda kesi hiyo, serikali ya awamu ya kwanza ya Tanganyika chini ya Rais Nyerere iliamua kufuta mifumo ya tawala zilizokuwepo kwa ajili ya kupoteza uhalali wa ushindi wa kesi mahak**ani aliyoipeleka Mangi Mkuu wa wachagga juu ya utawala wa umangi.

Hivyo mfumo wa utawala uliokuwepo Kilimanjaro uliokuwa umechanganyika na tamaduni za kichagga na demokrasia ndani yake ambayo k**a tulivyoona ilikuwa ni demokrasia yenye uwakilishi madhubuti kuannzia ngazi za chini kabisa za kiutawala iliyokomaa kuliko hata demokrasia iliyopo Tanzania ya karne ya 21, lakini ilifutiliwa mbali bila huruma bila hata kujali mapinduzi makubwa ya kihistoria ya kiuchumi na kisiasa iliyoyaleta Kilimanjaro kabla ya uhuru wa Tanganyika.

Baada ya mfumo wa kisiasa wa wazawa uliokuwepo kuondolewa mara baada ya uhuru wa Tanganyika ndio ukawa mwanzo wa Kilimanjaro kuletewa viongozi wa kuwaongoza na Rais wa Tanganyika kutoka maeneo mengine ya nchi k**a vile mkuu wa mikoa, wakuu wa wilaya, wakurugenzi wa halmashauri, makatibu tarafa n.k.,.

Viongozi hawa wa kuletwa na Rais wa Tanganyika/Tanzania kutoka nje ya Kiilimanjaro hawafahamu chochote kuhusu Kilimanjaro kuanzia historia yake katika nyanja zote za kijamii mpaka tamaduni zake na wakiwa hawajachaguliwa na wananchi wa Kilimanjaro hivyo hawana malengo wala maono yoyote juu ya Kilimanjaro zaidi ya kutimiza maslahi na matakwa ya kisiasa na ya kibinafsi ya aliyewaleta Kilimanjaro ambaye ni Rais wa Tanganyika/Tanzania.

Mkuu wa mkoa wa kwanza Kilimanjaro baada ya uhuru wa Tanganyika aliyeitwa Edward Barongo alikuja na mfumo mpya wa Tanganyika baada ya uhuru na hata mpaka leo Kilimanjaro haijawahi kabisa kuwa na mkuu wa mkoa ambaye ni mzawa wa Kilimanjaro na hata ikitokea akawepo bado ataishia kuwa kibaraka wa aliyemweka hapo madarakani kwa sababu atakuwa ameletwa tu na hajachaguliwa hivyo atalipa fadhila kwa aliyemleta.

Mfumo huu mpya wa utawala wa serikali ya Tanganyika/Tanzania nao umekuwa ni k**a tu ule wa kikoloni wa kuletewa viongozi wa kuwatawala badala ya kuchagua magavana wenu wenyewe kutoka hapo hapo Kilimanjaro ambao ni wazawa wenye kujua historia na tamaduni za Kilimanjaro na wenye uzalendo wa dhati kwa Kilimanjaro na ambao wako kwa ajili ya maslahi ya wananchi wenyewe wa Kilimanjaro tofauti na wale wa kuletewa.

Hata hivyo pamoja na kwamba mfumo wa wakoloni waingereza nao ulikuwa wa kuletewa gavana wa kuwatawala k**a jinsi ulivyo huu wa Tanganyika/Tanzania lakini bado mfumo wa kikoloni wa waingereza ulikuwa na nafuu kuliko huu wa serikali ya Tanganyika/Tanzania kwani angalau ule wa wakoloni waingereza haukuingilia moja kwa moja utawala wa ndani wa wazawa wala kuwaletea viongozi kutoka serikali kuu walioteuliwa na gavana wa Tanganyika k**a ilivyoanza kufanywa na Rais Nyerere baada ya uhuru wa Tanganyika, badala yake serikali ya wakoloni iliwaacha wazawa kutengeneza mfumo wao wenyewe wa kiutawala na kuchagua viongozi wao wenyewe.

Uhuru huu wa wachagga kujitawala wenyewe wakati wa serikali ya waingereza uliwapa fursa wachagga kupiga hatua kubwa kimaendeleo na Kilimanjaro kustawi vizuri na kwa viwango vya juu sana vilivyoweza kuteka umakini wa vyombo vya habari vya kimataifa kabla ya anguko kubwa la kiuchumi lililokuja baada ya uhuru wa Tanganyika kutokana na serikali pamoja na zile taasisi za wazawa zilizoleta maendeleo makubwa Kilimanjaro kuondolewa na kufutwa kabisa kwa hoja kwamba mambo yote yaliyofanyika kabla ya uhuru wa Tanganyika ni ya kikoloni na hivyo kila kitu kinatakiwa kufanyika upya bila kujali ni hatua kubwa kiasi gani ilikuwa imepigwa hapo kabla.

Hata suala la kusifia yaliyofanyika kabla ya uhuru wa Tangayika ilionekana ni kukosa uzalendo kwa serikali mpya ya Tanganyika/Tanzania na watu kwa kuogopa aibu ya kushutumiwa kwamba sio wazalendo waliacha kuzungumzia mambo mazuri yaliyokuwa yamefanywa na wachagga miaka ya kabla ya uhuru wa Tanganyika.

Lakini pamoja na yote hayo yaliyotokea sambamba na propaganda nyingi za kisiasa za kupuuza na kubeza yaliyokuwa yamefanyika, hata hivyo kamwe haziwezi kusahaulika hatua kubwa za kimaendeleo katika kila nyanja ya maisha ambazo wachagga walikuwa wamepiga chini ya utawala wa Mangi Mkuu wa wachagga akishirikiana kwa ukaribu na baraza la Halmashauri kuu ya wachagga.

Walisukuma mbele agenda nyingi za kimaendeleo kuanzia kiuchumi, kijamii na hata kutunza na kupigania utamaduni asili wa wachagga. Walijitahidi katika ujenzi na uboreshaji wa miundombinu ya barabara, mashule, vituo vya afya, tafiti mbalimbali za kisayansi juu ya kilimo, vyuo vya kisasa, miundombinu ya maji, umeme pamoja na kuwekeza kwenye biashara k**a za hoteli kwa ajili ya utalii wa mlima Kilimanjaro uliokuwa unaendelea kukua kwa kasi. Haya yalikuwa ni maendeleo makubwa kwa kipindi hicho kabla ya uhuru wa Tanganyika ambayo kamwe hayawezi kusahaulika wala kubezwa.

Chama cha kisiasa cha CDP kilichoongozwa na Eliufoo Solomon kilikuwa na sera zilizoweza kurubuni watu kwa maneno na ahadi kedekede zilizoweza kuhadaa wachagga kuunga mkono sera hizo kwa kupiga kura ya maoni dhidi ya sera za chama cha wachagga wahafidhina (KCCU) na kufanikiwa kushinda.

Hata hivyo Eliufoo Solomon na vijana wengine hawakuwa na sera zinazoeleweka kwa usahihi, na wala hawakuwa na maono wala mpango wa kufanyia kazi sera hizo baada ya kushinda kura husika ya maoni.

Licha ya kuzungumzia demokrasia ambayo tayari ilikuwepo kwa kiwango kikubwa Kilimanjaro kuliko hata iliyopo Tanzania ya leo, Eliufoo pamoja na watu wote wa chama cha TANU waliokuwa nyuma yake hakuna hata mmoja wao aliyekuwa na uzoefu wa kiuongozi katika nchi hapo kabla k**a alivyokuwa Mangi Mkuu wa wachagga, na wakafanya kazi katika hiyo demokrasia waliyokuwa wanainadi tofauti na chama cha (KCCU) waliokuwa wananadi mambo yaliyokuwa yanaendelea Kilimanjaro kwa wakati husika.

Pengine kukosa uzoefu kabisa ukichanganya na nguvu iliyokuwa nyuma yake vilichangia yeye Eliufoo Solomon kushindwa kufanya chochote baada ya kupewa ofisi ya urais wa wachagga na badala yake aliitelekeza ofisi aliyopewa na wachagga na kukimbilia Dar es Salaam ili kujumuishwa kwenye baraza la mawaziri la kwanza chini ya serikali ya awamu ya kwanza ya Tanganyika baada ya waingereza.

Kitendo cha Eliufoo Solomon kuondoka Kilimanjaro na kutelekeza ofisi aliyochaguliwa kilionyesha kwamba hakuwa na nia yoyote ya kukuza ustawi wa Kilimanjaro k**a alivyojinadi badala yake alikuwa ametumwa tu na hivyo kuhesabiwa k**a msaliti na zaidi mhaini.

Shutuma hizi za Eliufoo Solomon kuonekana k**a msaliti zilijidhihirisha wazi mwaka 1965 aliporudi Kilimanjaro kugombea ubunge wa jimbo la Hai kwa tiketi ya chama cha TANU ambapo kwenye kampeni zake huko Machame wapiga kura walimzomea na kumwita majina mbalimbali k**a vile msaliti, mhaini, mtu asiyeaminika, mtu asiyefaa wala wa kutegemea, ambapo yeye mwenyewe binafsi alishindwa kuwashawishi watu kwa hoja kuwa yeye sio msaliti kwa kitendo alichofanya cha kuhadaa wachagga na kuhujumu maendeleo ya Kilimanjaro.

Hali hii ilimtokea Eliufoo Solomon kwa sababu wachagga walitegemea kwamba baada ya chama cha CDP kupigiwa kura na kupewa ridhaa ya kukalia ofisi kubwa zaidi ya wachagga Kilimanjaro angekuja na mipango mikakati ya namna Kilimanjaro itasonga mbele kutokea pale ilipofika baada ya Mangi Mkuu kuondoka madarakani.

Hili ni jambo ambalo watu wengi walitarajia litatokea hata ikiwa Tanganyika itapata uhuru na Kilimanjaro ikiwa ndani yake kwani mfumo huo ungeweza kufanya kazi k**a vile ulivyokuwa unafanya kazi wakati serikali ya waingereza ikiwa katika madaraka na pengine mambo walitegemea yangekuwa mazuri zaidi kwao baada ya uhuru kwani serikali mpya ya Tanganyika/Tanzania ilipaswa kuja na mipango bora zaidi kwa maendeleo ya wazawa Kilimanjaro kuliko kipindi cha wakoloni k**a jinsi walivyokuwa wanaahidi kwa wananchi kabla ya uhuru wa Tanganyika.

Hata hivyo mambo yalienda kinyume chake k**a ilivyotokea baada ya uhuru wa Tanganyika ambapo hali ya kiuchumi Kilimanjaro ilidorora na kuendelea kuwa mbaya siku hadi siku mara baada ya uhuru wa Tanganyika.

Wachagga katika miaka ya 1960’s hawakuweza kumuelewa Eliufoo Solomon aliyejiunga na serikali ya Tanganyika/Tanzania ambayo ilipelekea maendeleo ya Kilimanjaro kudumaa tofauti na yalivyokuwa kabla ya uhuru wa Tanganyika kinyume na walichokuwa wanaahidi kabla ya uhuru wa Tanganyika.

K**a hiyo haitoshi serikali mpya ya Tanganyika/Tanzania pia ilifuta vyama vyote vya kisiasa ndani ya Tanganyika/Tanzania mara baada ya uhuru wa Tanganyika na kubakiza chama cha TANU peke yake ambacho kilikuwa kimekabidhiwa madaraka na waingereza na hivyo hata ile demokrasia ambayo Eliufoo Solomon na washirika wake waliitumia k**a propaganda ya kuingia na kuharibu mfumo wa uchumi Kilimanjaro ilidorora sana hata ndani ya Tanganyika yenyewe na hivyo ule uhuru wa kisiasa uliondoka sio tu Kilimanjaro bali hata ndani ya Tanganyika yenyewe chini ya Rais Nyerere mambo yaliharibika sana.

Eliufoo Solomon mwenyewe alikuja kufariki miaka kumi baadaye mwaka 1971 akiiacha nchi ya Tanganyika na hususan Kilimanjaro ikiwa katika sintofahamu kubwa kiuchumi na hata kisiasa kukiwa hakuna demokrasia aliyoitumia k**a propaganda sio tu ndani ya Kilimanjaro bali hata Tanzania kwa ujumla na hata maendeleo ya kiuchumi kudorora sana.

Ahsanteni.
CREDIT@ URITHI WETU WACHAGGA FACEBOOK PAGE

Address

Shanty Town
Moshi

Website

Alerts

Be the first to know and let us send you an email when Matukio Halisi posts news and promotions. Your email address will not be used for any other purpose, and you can unsubscribe at any time.

Contact The Business

Send a message to Matukio Halisi:

Videos

Share